Tuesday, July 29, 2008

YANGA YATIA AIBU YA KARNE KAGAME CUP

Hatimaye timu ya Tusker ya Kenya imeibuka ni mabingwa wa kombe la Kagame. Ni ushindi ambao umesisimua kwani wengi wa mashabiki walitarajia URA kushinda mechi ile. Kwa kweli mechi hiyo ilikuwa nzuri na iliyojaa ushindani japo URA walijisahau kwa kupoteza umakini katika dakika za mwishoni na kuruhusu wapinzani wao kujipatia mabao mawili ya haraka.
Kwa ufupi mashindano ya Kagame mwaka huu yalikuwa mazuri kwani naamini yaliandaliwa vizuri na kisasa kabisa. Kwanza yalichezwa katika kiwanja kizuri na pia nilishuhudia timu zikitumia vifaa bora vyenye nembo ya wadhamini. Si hayo tu, kila baada ya mechi kulikuwa kuna nafasi ya makocha kufanya mahojiano na wanahabari kitu ambacho kilitia hadhi ya mashindano na kuonesha angalau sasa ukanda wa Cecafa umeanza kujua nini kinatakiwa kifanyike katika kuandaa na kusimamia mashindano.
Kuna mambo kadhaa ambayo napenda niyatathmini kutokana na michuano ya mwaka huu. Moja, vilabu vyetu vikuu ndio chanzo cha kudumaza soka la Tanzania. Navisemea Simba na Yanga kwani utaona vilabu hivi vinawekeza fedha nyingi sana kununua wachezaji kutoka nje ambao viwango vyao ni sawa kabisa na wachezaji tulionao hapa. Sioni mantiki kununua wachezaji kutoka nchi jirani wakati vipaji tunavyo hapa nchini ila tatizo watu hawaishi Dar es salaam. Naamini kabisa nchi hii ni kubwa na ina uwezo wa kupata wachezaji wa kila nafasi.
Pili, pamoja na timu hizi kuwa na walimu kutoka Ulaya lakini bado utaona staili ya uchezaji si ile ambayo mtu ungetegemea wachezaji wetu waioneshe. Sioni jambo jipya hasa kwenye eneo la ufundi na mbinu (techniques). Utaona kabisa kwa mfano Simba ina uwezo mkubwa sana wa kucheza mpira mzuri wa kuonekana lakini hawana mbinu hata kidogo. Yanga nayo ndiyo basi huoni mbinu miongoni mwa wachezaji. Timu zote hizi mbili zinatumia zaidi mpira wa kiasili (traditional football) yaani kila mtu kucheza kwa namba na wala si kwa idara kama mpira unavyochezwa siku hizi. Ni mpira wa aina hii ambao hata Timu ya Taifa, ya Maximo mambo ndio hayahaya.
Tatu, ni hii habari ya mechi ya mshindi wa tatu, ambapo timu ya Yanga iligoma kufika kiwanjani kwa ubishani nadhani wa mgawanyo wa mapato. Ni fedheha kubwa kuwahi kulikumba soka la bongo. Mimi si shabiki wa timu hizi za Dar es salaam, ila siku ile Yanga walipogoma kufika uwanjani nilichukia sana na kujiona ni jinsi gani Tanzania kama nchi imefilisika kifikra. Yaani bila aibu, timu inaamua kujitoa mashindanoni baada ya kushindwa kukubaliana kifedha.
Hali hii ya Yanga kujitoa inanifanya nijiulize hivi kunani TFF? Umefika wakati maandalizi ya mashindano yawe na sheria kali na yasizipe nafasi timu fulani kuwa na sauti ya kimaamuzi juu ya suala la mgawanyo. Mambo yote yawekwe wazi kabla michuano haijaanza. Inakuwaje wakati michuano inaendelea katikati ndio makubaliano juu ya mapato yanafanyika? Hebu tuchukulie kwa mfano fainali iliyopita ya Kombe la Mabingwa Ulaya (Champions League) kati ya Manchester United na Chelsea. Fainali ya timu hizi mbili ilikuwa ni mojawapo ya mechi ambayo ingevutia watu wengi lakini hatukusikia UEFA wakianza kuvutana na vilabu hivi vikubwa vyenye mashabiki lukuki ulimwenguni. Hii ni kwasababu mwanzoni mwa michuano mambo yote yanakuwa yameshaamuliwa kwa mantiki ya kuzingatia mgawanyo wa mapato ambao hauwezi kuleta matatizo.
Naamini kabisa kama lengo la Cecafa ni kuinua kiwango cha soka katika ukanda huu basi ijiangalie ni jinsi gani inaweka mambo haya ya mapato sawa kabla ya mashindano. Na pia ufike wakati busara itawale tamaa zetu za kupenda fedha miongoni mwa viongozi wa vilabu. Yanga imetutia aibu kama Taifa manake hainiingii akilini viongozi kutokuleta timu uwanjani. Utafikiri hayo mamilioni waliyokuwa wanayalilia wangeyatumia vizuri. Hii ni timu inang’ang’ania mapato makubwa lakini huoni wanazifanyia nini. Ni timu ambayo ni kongwe lakini haina hata uwanja wa kisasa wa kufanya mazoezi ama hata ofisi za kisasa ambazo kama klabu ingepaswa ioneshe mfano.
Tatizo la Yanga karibu lifanane na lile la Simba kujitoa kombe la Tusker eti mgao lilikuwa tatizo. Mimi huwa nashangaa hawa viongozi wa vilabu vyetu hivi kwanini wanadai mafedha lakini hatuyaoni yakitumika kuleta tija kwenye vilabu? Hebu angalia Simba nayo hawana hata kiwanja cha mazoezi. Hivi klabu kama Simba ikiendelea kutembelea vilabu kama vile Sport Club Villa pale Kampala wataamini watakachokikuta pale kwenye kiwanja chake cha Villa Park? Nasema ni bora sasa tuwaulize wote waliowahi kuwa viongozi wa vilabu hivi wamevifanyia nini vilabu hivi? Kama sio ufisadi wa kimafia mafia tu hamna lingine zaidi ya kushibisha matumbo yao.
Tatizo la Tanzania ni kuwa wengi wa viongozi wa vilabu wawe ni wachezaji wa zamani ama hata mashabiki uchwara, hakuna kabisa utashi wa maendeleo ya jumla bali ni ubinafsi mtindo mmoja.
Kwa haya yalitokea kwa Yanga ni kielelezo tu cha jinsi gani nchi yetu imeporomoka kimaadili na tumbo zimewekwa mbele kuliko kitu kingine. Katika hali hiyo tusitegemee mpira kuendelea kirahisi hasa kutokea timu za Simba na Yanga. Tuanze kwenda mikoani na tuliimarishe soka la mikoani kwanza na haya mambo ya migao yatakwisha tu.
Mwisho, naamini Yanga lazima ipewe adhabu kubwa iwe ni fundisho. Na TFF iache haya mambo ya kuzilea hizi timu kubwa lakini zisizokuwa na lolote la kuigwa katika maendeleo ya soka la nchi yetu. Kwa vyovyot e vile yaliyotokea ni hii mazoea ya TFF kuziona Yanga na Simba kama Mungu na kuzitumia kama nguzo kuu ya kupata fedha. Kwa maana hiyo, kwasababu fedha ni muhimu kuliko chochote kwa TFF na vilabu hivi basi ndio maana haya yametokea. Inahitajika utendaji kazi wa kisasa (professionalism) ili tufike kisoka wenzetu walikofika.

Thursday, June 26, 2008

TAIFA STARS HAIKUWA NZURI SANA (Not good enough)

Najaribu kumfikiria na kumchambua Marcio Maximo pamoja na timu yake napata shida sana kuamua je tatizo ni kocha ama wachezaji? Nikitaka niwapongeze kwa jinsi walivyokufa kiume nashindwa manake naweza sema kuwa katika mechi zao mbili dhidi ya Cameroon kitu pekee walichofanya ni kuwabana Cameroon na kuzuia ama kuharibu mtiririko mziima wa uchezaji wa Cameroon.
Sikuona kama timu ya Taifa Stars ilikuwa na uchezaji wenye mfumo hasa. Kwa maana nyingine sidhani kwa uchezaji wa aina ile ningekuwa na fikira za timu kufuzu kwenda Angola ama Afrika Kusini. Timu yetu haina kiungo mchezeshaji (playmaker) na hivyo timu yetu imejengwa kwa kuegemea ulinzi tu. Tunacheza tukijitahidi tusifungwe wala hatushambulii kabisa na matokeo yake tunashindwa hata kupata ushindi wa mechi ndogo kama Mauritius. Ndio maana hadi leo hatuna mchezaji nyota hasa kwani huwezi kusikia kama fulani hayupo basi leo timu itapwaya. Ni lazima timu iwe na mchezaji ama wachezaji wachache mahiri ambao ni roho ya timu ndio tunaweza kufanikiwa ninaamini.

Hili nadhani ni tatizo la kitaifa manake hata nikitizama jinsi timu zetu za ligi kuu zinavyocheza mara nyingi huoni kama kuna mfumo ama kuna uchezaji wa mbinu za kupanga mashambulizi. Na mara nyingi si timu ya Taifa Stars tu bali hata Simba na Yanga pamoja na timu zote za Mikoa ambazo zilishiriki mashindano ya Taifa Cup sikuona mfumo kabisa.
Tunachoweza tu ni kulinda lango lakini unapoanzia idara ya kiungo cha ushambuliaji na ushambuliaji ni bure kabisa. Ni katika mtizamo huu nina wasiwasi hata tukimlaumu Maximo na akina Tinoco bado tunabaki tukijiuliza hivi Makocha wa vilabu vyetu wameshindwa nini? Kwanini wachezaji wetu si wabunifu? Hata pale timu inapokuwa nyuma kimchezo bado hatuoni mchezaji hata akijaribu basi kupambana kwa juhudi binafsi. Ni hatari sana kwa uchezaji wa aina hii kwani inatia shaka kama kweli wachezaji wetu wana moyo wanapoichezea timu ya Taifa.
Soka ya Tanzania inachezwa na magazeti sana kwa kuwadanganya wachezaji wetu kuwa wapo juu. Nina mifano miwili hapa: Ngassa kapigiwa sana debe kuwa ni mahiri lakini alipopewa nafasi dhidi ya Cameroon imedhihirika kuwa bado ana safari ndefu sana hasa kimbinu na nguvu. Hana nguvu kabisa na katika mechi dhidi ya Cameroon mara nyingi alishindwa kujua acheze namna gani dhidi ya wachezaji wenye maumbo makubwa. Sidhani kama ilikuwa ni busara kwake kucheza karibu sana na mpinzani ukizingatia ana kasi lakini mara nyingi alikuwa anakaa na mpira kumsubiri adui nah ii ilimshinda.

Mfano wa pili ni kuhusu jinsi mabeki wetu wa pembeni wanavyocheza: sipendi kabisa uchezaji wa kizamani ambao nimeushuhudia katika mechi zote hadi sasa. Beki kama Nsajigwa ana uwezo mkubwa wa kupanda mbele na kushambulia. Nadhani ukizingatia tuna beki mwingine mzuri wa kulia …………… basi ingekuwa vyema upande wa kulia tuwatumie wote upande wa kulia na ninaamini mambo yangekuwa mazuri.
Kitu kingine ambacho naamini kwa timu changa na isiyo na uzoefu kama yetu ingefaa ikizingatie basi ni upigaji wa mashuti ya mbali. Wachezaji wetu hawapigi mashuti ya mbali kabisa wanataka kupenya ngome ya adui wakati hawana uwezo wa kupasiana na kubadilishana mpira ipasavyo.
Si kupasiana tu ila kuna upigaji vichwa na matumizi ya kifua katika kumiliki mpira. Mara nyingi wachezaji wetu wanaonekana kabisa hawajui kupiga vichwa wala kutumia kifua katika kucheza mpira. Mpira wa juu wowote utaona wanaucheza kwa woga na mara nyingi mtu akipiga kichwa anapeleka kwa adui. Nadhani kwa makocha wa vilabu vyetu ni lazima hili lifanyiwe kazi manake ni balaa kwa wachezaji wa kitanzania. Hata hii michuano ya Coca Cola kwa vijana nimeona hili ni tatizo kabisa. Inaonekana walimu wetu hawazingatii mambo kama haya ambayo ni muhimu sana kwa mchezaji kuweza kumudu mechi zenye wachezaji wa kiwango cha wale wa kulipwa Ulaya.
Jambo lingine ni kuwa sasa umefika wakati tuangalie mfumo wa waamuzi wetu kupenda virushwa kwani ni wazi wachezaji wetu hasa wa vilabu vikubwa wamezoea kubebwa na inawawia vigumu kuweza kumudu mechi za kimataifa ambazo ni mara chache mchezo mchafu kuwezekana.

Yapo ambayo yanatakiwa yafanyike kwani kila kitu kinawezekana. Mosi ni vyema Ligi Kuu iimarishwe kwa kuzingatia viwango (standards) na kutoruhusu mizengwe na upendeleaji wa mara kwa mara kwa vilabu vikubwa; hii haisaidii sana soka letu. Pili, TFF ipanue wigo wa kupata wachezaji mahiri kwa kuhakikisha kunakuwa na Ligi Daraja La Kwanza ambayo itaongeza wigo wa kupata wachezaji kwenye timu ya Taifa. Hii itasaidia hasa kuwanyanyua wachezaji wenye vipaji adimu mikoani ambako ni vigumu kuweza kuonwa tu na vilabu vya ligi kuu.
Labda niseme tu sikutarajia kama tungefuzu hasa pale tulipopoteza mchezo dhidi ya Mauritius hapa nyumbani. Hatukustahili sare kabisa na nadhani umefika wakati wachezaji wetu wajue kuwa mchezo wa nyumbani ni lazima washinde; na timu yeyote inayoshindwa kupata ushindi nyumbani basi imepoteza nafasi ya kufuzu mashindano. Ndio maana baada ya mechi ile nilijua basi tena tumekwisha. Lazima wachezaji wetu waige kwa majirani zetu Kenya, Uganda na Rwanda jinsi wanavyohakikisha hawashindwi mechi za nyumbani. Pale tu tutakapoweza kushinda mechi za nyumbani basi tutakuwa na nafasi ya kufuzu mashindano yeyote yale.

Mwisho kabisa najiuliza hivi kweli wachezaji wetu huwa wanatizama mechi za ligi za Ulaya na kufuatilia kwa dhati? Inaonekana kabisa bado hata masuala madogo madogo ya kiuchezaji hasa mbinu kwao ni taabu sana. Mara nyingi naangalia jinsi ambavyo wanavyoshindwa hata kujipanga wakati wa kupiga mipira ya adhabu inanikera sana. Natoa rai kwa wachezaji wetu kama kweli wanaupenda mpira basi wafuatilie nini kinafanywa na wenzao wa huko Ulaya.
Nimalizie kwa kuitakia Taifa Stars iweze kuifunga Sudan mwezi wa September ili angalau basi tuweze kufuzu kwenda kwenye fainali za wachezaji wasio wa kulipwa Ulaya. Hii itakuwa ni hatua moja mbele kwa wanasoka wa kizazi cha leo na ambayo itatusaidia kupata hata nyota wachache watakaouzwa huko Ulaya. Manake bila kuwa na wachezaji wa kulipwa Ulaya tutaendelea kuwa wasindikizaji tu. Wenzetu majirani Uganda wanafanya vizuri tu.
Unaweza kuona ndio maana kwa sasa hadi raundi hii ya nne inamalizika msimamo wa kundi letu unaonesha jinsi tulivyo taabani kwa matokeo ya mechi tulizokwishacheza:
01-02/06/08: Cameroon 2-0 Cape Verde 01-02/06/08: Tanzania 1-1 Mauritius
06-08/06/08: Cape Verde 1-0 Tanzania 06-08/06/08: Mauritius 0-3 Cameroon
13-15/06/08: Tanzania 0-0 Cameroon 13-15/06/08: Mauritius 0-1 Cape Verde
20-22/06/08: Cameroon 2-1 Tanzania 20-22/06/08: Cape Verde 3-1 Mauritius
Msimamo mzima wa makundi yote waweza kuusoma jinsi ulivyo hapa hadi raundi ya nne.

Thursday, June 19, 2008

STARS WAENDA CAMEROON

Taifa Stars hatimaye wanaondoka asubuhi hii. Kitu pekee nachadhani kitasaidia kupata bao ni upigaji mashuti ya mbali.

Wednesday, June 18, 2008

JIWANJA LETU MALI SANA

Leo nawaletea jinsi nilivyoshuhudia uzuri wa Jiwanja letu.
choo ndani
Wadau kabla ya kuingia kiwanjani
sehemu ya nje
Magari nje utadhani majuu
Sehemu ya kunawa mikono mdau akijisafisha.

Tuesday, June 17, 2008

Raundi Ya Tatu

Raundi ya Tatu wiki iliyopita ilituumiza zaidi watanzania baada ya kushindwa kupata point tatu kwa Cameroon. Raundi msimamo wa makundi uko hivi:

Sunday, June 15, 2008

USHUHUDA NA BONGO SOKA UWANJA MKUU WA TAIFA

Bongo soka ilishuhudia mechi ya jumamosi. Hapo chini nipo na mdau mwenzangu tukijiaandaa kuingia. Shuhudia hali ilivyokuwa katika picha.

Hapa wadau tukiwa nje ya lango kuu


Ninafuatilia mechi hapo juu kwenye viti vya makabwela (5000/=)

Nje ya uwanja kunavyoonekana

Kwa nje, gari ya Kamanda Kova ilipaki ndani ya jiwanja

Kiwanja kilijaa pomoni.Hapa nyimbo za Taifa zinapigwa

TAIFA STARS 0 - CAMEROON 0

Hapo juu ninaangalia mechi hiyo ya jumamosi
Mechi ya juzi kati ya Taifa Stars na Cameroon, niliishuhudia kama mdau wa soka wa Tanzania. Kwa ufupi sidhani kama Cameroon walicheza mchezo wao hasa na hawakuonesha sana kutaka kufunga kwa kila juhudi. Hali hii iliiweka timu yetu katika wakati mgumu lakini naamini kama watashambulia mechi ijayo basi Stars watapata nafasi ya kuwakamata na kuuwafunga.

Kama tutashinda mechi hiyo basi ndoto za kufuzu zitakuwa zimerejea japo kwa sasa mimi sina matumaini.

Sunday, June 8, 2008

RAUNDI YA PILI ILIVYOKUWA

Wikiendi hii matokeo ya mechi zote yalikuwa kama ifuatavyo:
Tanzania ililala mbele ya Cape Verde 1-0 kwa bao la Babanco. Cameroon ikaichabanga Mauritius 3-0 kwa mabao ya Andry Bikey, Etoo na Bebey Mbangue Gustave.
Kundi la Pili Zimbabwe iliichapa Namibia kwa 2-0 mabao ya Gilbert Mushanghazike. Zimbabwe imejaza mastaa wa nchi za Ulaya na Afrika Kusini sio timu ya kubeza.
Kenya waliwachabanga Guinea bao 2 - 0. Uganda wakabumundwa bao 4 - 1 na Benin baada ya uzembe wa golikipa Dennis Onyango. Rwanda wakawalaza Ethiopia ugenini 2 - 1. Burundi wakalazwa na Burkinafaso. Kwa ujumla hadi sasa matokeo ya raundi mbili ni:

KICHWA CHA MWENDAWAZIMU 0 – CAPE VERDE 1

Hatimaye michuano ya kufuzu kwa fainali za Kombe la Dunia za mwaka 2010 huko Afrika ya Kusini pamoja na zile za Mataifa ya Afrika kule Angola zimefikia raundi ya pili. Kampeni za Tanzania, Taifa Stars zimeendelea kusuasua kama nilivyobashiri kuwa itakuwa ni mechi ngumu sana. Hawa mabwana wa Cape Verde wameifunga Taifa Stars kwa bao moja bila majibu.
Cape Verde nawakumbuka vizuri walicheza na Harambee Stars katika harakati za kufuzu michuano iliyopita na waliipa shida sana timu ya Kenya katika mechi ya marudiano. Hivyo nilitaraji tutapata taabu sana. Sidhani ni wakati wa kumlaumu mtu yeyote kwani nilifuatilia mechi ile redioni na ninaweza kusema tumefikia ukomo wetu kama Taifa. Aina ya wachezaji tulionao hata aje Scolari ama Erickson hapa bongo, ni kwamba tuna safari ndefu sana katika soka. Na kwasababu hatutaki kuamini ukweli huu, basi hatutaendelea kisoka kabisa.

HATUNA ‘QUALITY PLAYERS’

Kwanini ninasema hivi? Mosi, Kocha Marcio Maximo anapigiwa kelele sana eti hana uwezo na ndio chanzo cha kufungwa kwetu. Mimi tangu aje nchini kwetu sikubaliani na hoja za wanaojiita wadau wa soka la bongo hata kidogo. Naamini maamuzi mengi ya Maximo ni kitaalam zaidi na ambayo kwa wengi wa watanzania hawayajui wala hawayataki. Watanzania wengi wanapenda mambo ya kienyejienyeji yasiyozingatia taratibu za fani husika. Kwa mfano, kuna wachezaji ambao wanapigiwa upatu waitwe kwenye timu hii lakini ukitizama kwa kina unaona kuna msukumo wa unazi wa “usimba na uyanga” katika madai ya wadau wengi.
Pili, suala la nidhamu ya wachezaji wetu ni tatizo la elimu miongoni mwao. Kwa uelewa wangu wa soka la bongo, wachezaji wetu wengi ni wale ambao ama wameacha shule na kujikita kwenye soka kama njia fupi kufikia mafanikio ya kimaisha. Wengine walifukuzwa shule kwa utovu wa nidhamu na wengi wao ni watumiaji wa vilevi mbalimbali ambavyo ni kinyume na maadili ya kimichezo. Kwa ujumla kandanda la bongo limejaa makapi kutoka katika fani nyingine na ndio hapa ninapoona uozo wa wachezaji wetu na sishangai hasa wachezaji wanapofukuzwa kambini ama wengine wanapokataliwa kuitwa timu ya Maximo licha ya kelele za wadau wengi ambao hata wao hawajui kanuni za soka kwa undani.
Tatu, kuna suala la kuwa je tuna wachezaji nyota Tanzania? Kwangu nadhani niseme hatuna na bado tuko kwenye mwanzo wa kuwavumbua. Hebu tujiulize maswali kadhaa: Je kwanini hatuna wachezaji wanaocheza soka la kulipwa Ulaya? Kama kwele vilabu vyetu kila mwaka vimeshiriki mashindano ya Afrika na hata timu yetu ya Taifa imeshiriki michuano ya kimataifa inakuwaje hatuvutii mawakala wa timu za nje ambao huwa wanakuwepo kutafuta nyota wa kuwanunua? Jibu ni kuwa wale tunaodhani ni nyota bado si nyota kwa viwango na vigezo vya kimpira vya kileo. Sisi tunawapima kwa vigezo vya kitanzania basi tunawaona kama malaika! Masikini wakubwa wa mawazo na upeo wa soka ndio ugonjwa unaotukabili haswa.
Nne, ningependa nitoe rai kwa watanzania kuwa tuache njozi na kufuata hisia zaidi ya hali halisi na kukubali ukweli. Nasema hivi kwani nina mifano kadhaa kuonesha jinsi soka yetu inavyoegemea zaidi hisia (fantasy) kuliko uhalisia. Nitoe mfano wa wachezaji wawili: Juma Kaseja na Athuman Machupa. Haipingiki kabisa kuwa Kaseja ni kipa bora kabisa hapa nchini na ni vigumu kumwelewa Maximo kutokumtumia wala kumwita timu ya Taifa. Lakini huwa najiuliza kitu kimoja kumhusu Kaseja: Kwanini kwa muda wote ambao amecheza soka hapa nchini hasa mechi nyingi za kimataifa inakuwaje hajawahi hata kuitwa kufanya majaribio ya soka la kulipwa katika vilabu vikubwa vya Afrika ya Kaskazini ama vile vya Afrika ya Kusini?
Katika mechi alizocheza alipata nafasi tosha kabisa kuonesha uwezo wake katika nchi mbalimbali lakini bado hakwenda japo hata hapo Rwanda ama Uganda. Hii inanifanya nimwone Kaseja kama mchezaji mahiri lakini kiviwango hapitani ama hapishani sana na wanasoka wengine ambao ni magolikipa hapa Tanzania. Yaani namaanisha umahiri wake si ule tunaoweza kuuita usio kifani. Na hili Maximo analijua ndio maana haangaiki labda.
Ukija kwa Athuman Machupa, huyu alipigiwa kelele sana eti aitwe time ya taifa na aliitwa na akashindwa kumthibitishia Maximo amwite tena. Ila kwangu kuna wakati nilisikia alikuwa nchini Uingereza akifanya majaribio ya soka kule nikasema sasa tutapata nyota. Lakini kwa mshangao nikasikia yuko Rwanda leo yuko Simba na mara nyingine yuko Mchangani. Je kama sisi tunamwona kama nyota lakini Uingereza tena madaraja ya chini kashindwa kufuzu majaribio, hapo tutaendelea kumpigia Maximo makelele amwite eti kwasababu ya hisia tu?
Mifano hiyo miwili ni kujaribu kuonesha jinsi gani soka letu bado liko usingizini na tunahitaji muda mrefu ili kuweza kufika pale tutakako. Tukiacha kuheshimu hisia basi tutafika lakini pale tutakapomfukuza Maximo na kufikiri tukirejesha kuendesha soka yetu kienyejienyeji kamwe hatutakaa tufike.

MATUMAINI YA KUFUZU YAPO?

Ni wazi kama mtanzania yeyote anafikiri tunaweza kufuzu kwenda Angola ama Afrika ya Kusini basi huyo hajui soka. Ili timu ifuzu kwenda kombe la dunia ni lazima nchi iwe na angalau klabu moja yenye mafanikio kisoka katika michuano ya kimataifa ambayo ndio itakayokuwa roho ya timu ya Taifa. Chukulia mifano ya nchi kama Angola, Tunisia, Misri, Libya na hata Benin ambazo wachezaji wake wengi ni wa ndani ya nchi. Huwezi kufuzu michuano mikubwa kama uendeshaji wa vilabu ni wa kienyeji ukifanyika katika vilabu vya pombe na kahawa chini ya watu wanaojiita marafiki wa klabu.
Nimalizie kusema tu kuwa kwa matokeo ya Cape Verde, basi naamini timu yetu imepoteza mwelekeo na sidhani kama tunaweza kufuzu labda tu tuifunge Cameroon hapa nyumbani wikendi ijayo na tuhakikishe hatupotezi tena wala kutoa sare mechi zijazo. Kinyume na hapo, timu ya Maximo kwa sasa ni kuendelea kulea kufundisha wachezaji wetu namna ya kusakata gozi. Ufike wakati wadau wa soka wafungue macho na kuona mbele. Tatizo si kocha wala upangaji wa timu, nadhani hatuna wachezaji wa kucheza soka la kiwango cha wapinzani wetu. Ukweli ni kuwa tujiulize kwanini wachezaji wetu nyota wanaishia Uarabuni kule ambako wanakwenda wachezaji wastaafu wa soka toka Ulaya?
Natoa rai, tusitafute mchawi hapa ila turidhike na matokeo na tuhangaikie zaidi timu za vijana kwani kwa sasa kazi ya Maximo ni kuvumbua vipaji kwa ajili ya baadaye sana. Tuangalie uendeshaji wa mchezo huu ngazi za mikoa na wilaya ndiko kwa kuanzia. Mungu Ibariki Tanzania.

Thursday, June 5, 2008

FAINALI ZA KOMBE LA DUNIA 2010 ZAANZA RASMI

Hatimaye michuano kuwania nafasi ya kufuzu kucheza fainali za Kombe la Dunia za mwaka 2010 huko Afrika ya Kusini zimeanza. Hizi ni fainali za kufuzu pia kwa kombe la Mataifa ya Afrika huko Angola hapo mwaka 2010. Hii ni makala ya kwanza ya ufunguzi wa blog hii ambayo itajikita katika masuala ya soka kwa ujumla wake. Nitachambua fainali hizi kwa undani hasa.
Kwa maana hiyo Timu ya Taifa ya Tanzania, Taifa Stars ilianza michuano hii kwa balaa kwani ilitoka sare na Timu ya Mauritius ambayo ilikuwa ni dhaifu sana. Wakati naandika waraka wa leo ndio timu imeondoka alfajiri ya leo kuelekea huko Cape Verde.
Katika mchezo ule kiwango cha uchezaji kilikuwa cha chini sana hasa katika kiungo cha ushambuliaji kwani inaonekana wazi kabisa hatuna mchezaji wa kuchezesha timu na kugawa pasi za mwisho kwa wafungaji. Wafungaji wanapewa pasi fyongo mara zote na inakuwa vigumu kufunga kwa urahisi. Ni lazima Maximo atafute wachezaji wa aina ya akina Messi ama Fabregas ili kuweza kuwatisha walinzi wa timu pinzani kurahisisha upenyezaji wa mipira yenye tija.
Ilikuwa ni mechi ya 25 kwa Maximo kama kocha akiwa na rekodi ya kupoteza mechi tano na kushinda mechi na kutoka sare 11. Ni rekodi nzuri. Katika mechi hii ya kwanza kwa michuano Maximo alitumia wachezaji wafuatao: Ivo Mapunda, Fred Mbuna, Maftah, Sallim Sued, Harob Canavaro, Godifrey Bonny, Henry, Emanuel Gabriel, Ulimboka, Jerry Tegete, Kigi Makassy, Athuman Idd na Nizar Khalfan.
Sijui atabadilishaje timu yake mechi ijayo tusubiri tuone.
Binafsi naamini kama kuteleza basi hapa ndio penyewe japo naamini ili tujisahihishe ni lazima tushinde mechi ya Cameroon hapa nyumbani wiki mbili zijazo na pia mechi ya Cape Verde wikiend hii. Tusiposhinda mechi hizi mbili basi kufuzu tusahau kabisa kwani ili tufuzu lazima tuwafunge Cameroon.
Kushindwa kuifunga Mauritius kulisababishwa na aina ya wachezaji tulionao hapa Tanzania. Naamini wachezaji wetu hawaangalii mipira mikubwa katika televisheni na kama wanatizama basi wanatizama picha na huwa hawasikilizi maoni ya watangazaji (commentaries) kwani huwa yanakuwa yamesheheni ushauri wa kitaalam ambao kwa vijana wetu kama wakifuatilia basi watafika mbali sana.
Haiwezekani unacheza nyumbani alafu unashindwa kufunga magoli hasa ukizingatia upinzani ulicheza na wachezaji kumi kwa muda mrefu. Timu yetu wachezaji wengi hawatumii akili kabisa. Sikufurahishwa na upigaji wa krosi nyingi ambazo hazikuwa zinalengwa kwa wafungaji bali kupiga tu kwa nguvu ili mfungaji autafute kitu ambacho naamini ni kigumu sana.
Maoni yangu ni kwamba Taifa Stars haijui aina ya uchezaji ya watu kama David Beckham ama Fabregas ambao upigaji wao wa pasi unakuwa ni kupeleka mpira kwa mtu na si kuupiga tu kwa nguvu ili mtu akutane nao. Mpira wa krosi sharti uwe umelengwa kwa mtu (intended to) na si kujipigia tu. Kama hatutaacha aina hii ya uchezaji basi tusijidanganye hata aje nani hapa bongo tutakuwa tunasikitika sana kila michuano.
Katika fainali hizi majirani zetu Kenya watacheza na Guinea chini ya Paschal Feundono wakati Uganda iko Benin ikicheza huko.
Nimalizie kwa kusema kuwa mechi ya wikiendi hii itakuwa ngumu kwani hawa Cape Verde si timu ya kubeza hata kidogo. Ni timu ambayo iliihangaisha sana Kenya katika michuano iliyopita na ina kiwango cha juu cha soka. Ninaamini kama TFF na akina Maximo wana utashi wa dhati na kazi yao watakuwa wameshawatizama hawa Cape Verde kupitia mikanda ya mechi zao walipocheza na Kenya katika fainali za Mataifa ya Afrika zilizopita kwani ni rahisi kuzipata kutoka kwa jirani zetu.
Mwisho niitakie Taifa Stars ushindi kwa mechi ya kesho.